WAZIRI MKUU AWAONYA VIKALI VIONGOZI WANAOGAWA MAENEO YA STENDI YA KANGE

Waziri Mkuu

     WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameonya viongozi wanaogawa maeneo kwenye kitega uchumi kipya cha Dkt. Samia Suluhu Hassan Business Centre kilichopo stendi ya Kange, nje kidogo ya Jiji la Tanga wajiepushe na vitendo vya rushwa.

     “Viongozi wote mnaosimamia mchakato wa kuwapata wapangaji wa jengo hili, jiepusheni na vitendo vya rushwa kwa kisingizio cha kutokidhi vigezo. Mkuu wa Mkoa upo hapa, wewe pamoja na watendaji wako hakikisheni mnachukua hatua stahiki. Fanyeni uhakiki wa vigezo vilivyopo ili kuwezesha wananchi wengi wenye nia kunufaika,” amesema.

    Ametoa onyo hilo leo (Jumatatu, Aprili 22, 2024) wakati akizungumza na viongozi na wananchi, mara baada ya ya kuweka jiwe la msingi la mradi wa kitega uchumi kilichopo eneo la Kange ikiwa ni sehemu ya shamrashamra za maadhimisho ya miaka 60 ya Muungano wa Tanzania ambapo kilele chake ni April 26, 2024.

     “Kwenye ugawaji wa maeneo kama haya, kuna watu huwa wanadai rushwa, mtu hata biashara yenyewe hajaanza, unataka atoe chochote, mtaji utabakia kweli?,” alihoji na kuwataka wananchi wakati wakifanya maombi yao wasisite kutoa taarifa iwapo wataombwa rushwa na maafisa wa Serikali ili wahusika wakamatwe.

      Amesema azma ya Serikali ni kuhakikisha kuwa halmashauri zote zinajiendesha na zinajisimamia kwa kutumia mapato yake ya ndani. “Ili kufanikisha azma hiyo, Serikali iliweka mikakati mbalimbali kwa ajili ya kuzigharimia halmashauri ambazo zilibuni miradi ya kimkakati yenye lengo la kutoa huduma bora zaidi na zenye uhakika kwa wananchi. Mradi wa kimkakati wa kitega uchumi wa Jiji la Tanga, ambao leo hii nimeuwekea jiwe la msingi ni moja ya miradi hiyo,” amesisitiza.

 

stories
standard
 
The subscriber's email address.
Stay informed - subscribe to our newsletter.